Ukiuliza ni wilaya gani miaka ya nyuma ilisumbuwa sana kwa bata na sehemu nyingi za mapumziko ndani ya jiji la dar es salaam kabla ya kuongezeka kwa wilaya za Ubungo na Kigamboni basi Kinondoni ilikuwa kiboko yao japo kwa sasa unapozungumzia fukwe za Bahari nzuri na nyingi lazima uanze na wilaya ya Kinondoni.
Manispaa ya Kinondoni imebarikiwa kuwa na eneo kubwa la fukwe safi na tulivu katika Pwani ya bahari ya Hindi kuanzia maeneo ya Oysteybay (Coco beach), Kawe beach, Mbezi beach, Kunduchi hadi Ununio.
Maeneo haya ya fukwe yana madhari nzuri kwa ajili ya mapumziko kwa kuwa na upepo mwanana wa bahari. Fukwe pia huwawezesha wakazi wa Jiji la Dar es Salaam kushiriki michezo mbalimbali ya kwenye maji ikiwemo kuogelea, matembezi, riadha, burudani n.k.
Kunduchi Beach yenye mabwawa makubwa ya kuogelea pamoja na Uwanda mkubwa wa Bahari unaotumika kwa michezo ya kukimbizana kwa pikipiki za majini ni kivutio kikubwa cha utalii katika Manispaa ya Kinondoni. Katika hoteli hii kuna maeneo yaliyotengenezwa kwa ajili ya michezo ya watoto na migahawa ya vyakula ambavyo hutia hamasa kutembelea maeneo haya.
Wakazi wa Jiji la Dar es Salaam na wageni mbalimbali pia wanapata fursa ya kufanya utalii wa bahari kwa kutembelea visiwa vilivyopo katika bahari ya Hindi vikiwemo Bongoyo, Pungavini, Mwakatumbe, Mbudya, na Sinda.
Vyakula safi vya asili ikiwemo samaki, vinywaji pamoja na michezo ya kwenye maji kwa kutumia vifaa maalum zikiwemo boti ni burudani tosha kwa wakazi wa Jiji la Dar es Salaam na wageni mbalimbali wanazozipata kwa uwepo wa fukwe.
#KonceptTVUpdates