Malawi imeomba msaada ili iweze kusambaza chakula kwa zaidi ya wakimbizi 50,000 wanaokabiliwa na uhaba katika kambi pekee ya wakimbizi nchini humo, wakati maafisa wa serikali wakisema akiba ya chakula itakwisha kufikia mwezi Desemba.
Ombi hilo limetolewa baada ya shirika la Chakula Duniani ,WFP kupunguza usambazaji wa chakula kwa wakimbizi hao, kutokana na kupungua kwa ufadhili. Wakimbizi hao kwenye kambi ya wakimbizi ya Dzaleka wanasema uhaba wa chakula umekuwa mbaya sana kwa sababu ya kuendelea kuwahamisha wakimbizi sehemu nyingine, ambao wamekuwa wakikaa nje ya kambi.
Serikali ya Malawi ilianza kuwahamisha wakimbizi na waomba hifadhi mwezi Juni kwa mujibu wa sera ya wakimbizi, inayowataka kuishi na kufanyia shughuli zao ndani ya kambi. Maafisa wa serikali wanasema kwamba zaidi ya wakimbizi 2,000 miongoni mwa 8,000 waliolengwa tayari wamehamishiwa kwenye kambi.
Mwezi uliopita, WFP ilipunguza mgao wa chakula kwa wakimbizi kwa nusu kutokana na matatizo ya ufadhili, wakati ikiomba msaada wa dola milioni 6.3, ili kukidhi mahitaji ya chakula kwa wakimbizi hao hadi Juni mwaka ujao.
Waziri wa Usalama wa ndani wa Malawi, Ken Zikhale Ng’oma wiki hii Jumatano wakati akihutubia wanahabari amesema kwamba hatua ya kupunguzwa kwa misaada ya chakula imeiacha serikali katika hali ngumu.
Dzaleka ni kambi iliyo na zaidi ya wakimbizi 50,000, huku wengi wao wakiwa ni kutoka Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo, Burundi, Rwanda, Ethiopia na Somalia. Hata hivyo uhaba wa chakula kwenye kambi hiyo umewalazimisha baadhi ya wakimbizi walioletwa kambini humo kurudi kwenye maeneo yaliyo nje.
#KonceptTvUpdates