Taasisi ya Vodacom Tanzania Foundation imetangaza leo septemba 13,2023 ushirikiano na waendesha baiskeli mashuhuli wa Twende Butiama kama mdhamini mkuu wa tukio lao la mwaka la Ziara ya Baiskeli itakayoanzia Dar es Salaam mpaka Butiama.
Tukio hili la uendeshaji wa baiskeli litakalodumu kwa siku 14, linatarajiwa kufanyika kuanzia Oktoba mosi mpaka Oktoba 14, 2023, likitumika kama heshima ya Maisha na kumbukumbu ya kumuenzi Hayati Baba wa Taifa, Mwl Julius Kambarage Nyerere, mtu muhimu katika historia ya Watanzania.
Gabriel Landa, Mwanzilishi Mwenza wa ziara ya Twende Butiama, ameelezea shukrani zake za dhati kwa taasisi ya Vodacom Tanzania Foundation. “Safari yetu ambayo imeanza mwaka 2018, inaenda mbele zaidi ya kuadhimisha kumbukumbu ya Baba wa Taifa. Tunahamasisha uendeshaji wa baiskeli – kitu ambacho Mwalimu alikipendelea zaidi – pamoja na kuwa vinara wa masuala ambayo aliyapambania kama vile elimu, utunzaji wa mazingira, na afya. Kwa ushiriki wa sekta binafsi na ushirikiano wa waendesha baiskeli, wanaharakati wa mazingira, na wataalamu wa afya, mchango wetu unalenga kuenzi maadili ya Mwalimu,” alisema Landa.
Urithi wa tukio la Twende Butiama kwa miaka mitano sasa limekuwa likiangazia masuala yanayogusa mazingira kwa kufanikisha kampeni ya upandaji miti.
Kwa kuongezea, jitihada za kuchangisha fedha kupitia kampeni ya “Changia Dawati, Tokomeza Ujinga” zinaonyesha kujizatiti katika elimu, kuwezesha usambazaji wa madawati takribani 200 katika shule za msingi 6 kwa mikoa ya Pwani, Morogoro, Dodoma, na Mara.
Akizungumza wakati wa mkutano na waandishi wa Habari, Mkurugenzi wa Vodacom Tanzania Foundation, Zuweina Farah amesema kuwa, “tunayo furaha kubwa kuujulisha umma kuwa tumedhamini Ziara ya Baiskeli ya Twende Butiama kama mdhamini mkuu kwa mwaka huu. Ushirikiano huu ni zaidi ya udhamini; ni muunganiko wa maadili, kujitolea, na kujizatiti kuwatumikia jamii ya Kitanzania kwasababu wakati wa ziara tutajihusisha na shughuli mbalimbali zinazolenga kuendeleza na kuenzi kumbukumbu ya Maisha ya Mwalimu.”
Mbali na kuchangia zaidi ya shilingi milioni 57 kuunga mkono shughuli za uendeshaji kwa ajili ya waendesha baiskeli, pia Vodacom Tanzania Foundation imejizatiti kushiriki kwenye shughuli tofauti zinazoendana na malengo mkakati yanayolenga kuleta mabadiliko kwa kuboresha huduma za afya, upatikanaji wa elimu bora, na uwezeshaji wa kiuchumi.
“Pia tutaungana na waendesha baiskeli wa Butiama kuchangia madawati kwa shule za msingi 5 na kupanda miti zaidi ya 2000 katika mikoa tofauti ambayo waendesha baiskeli watapitia. Shughuli hii inaendana na shauku ya mpango wetu wa kupanda miti milioni 2 nchini kote ifikapo mwaka 2030. Kwa kuongezea, tunashirikiana na ‘Afya Checkers’ ambao ni wataalamu wa huduma ya afya kuandaa kambi ya kutoa Huduma ya Matibabu ya bure katika mikoa ya Mwanza, Bunda, na Butiama ikiwa ni juhudi zetu za kupambana na magonjwa ya kuambukiza nchini Tanzania vilevile kuchangia vifaatiba kwa Hospitali ya Wilaya ya Butiama,” alisema Bi. Farah.
Kwa upande wake Dkt. Isaac Maro akizungumza kwa niaba ya wataalamu wa afya ambao watakuwa sehemu ya ufanikishaji wa Kambi ya Matibabu ya bure ameishukuru Vodacom Tanzania Foundation kwa kuwaunga mkono kuhakikisha zoezi la kambi hiyo linafanikiwa kwa wakazi wa Mwanza, Bunda, na Butiama.
“Tunayofuraha kuwa sehemu ya Ziara ya Baiskeli ya Twende Butiama kuenzi kumbukumbu ya Mwalimu kupitia uwezeshaji wa kambi ya matibabu ya bure. Mwalimu alijitolea kupambana na magonjwa nchini Tanzania na tunatarajia kusaidia na kuwahudumia watu wengi kadri tuwezavyo. Tutakuwa na wataalamu wa afya watakaowahudumia na kuwashauri watu ambao watahudhuria. Ningependa kutoa wito kwa washirika wengi kujitokeza zaidi kuunga mkono jitihada hizi za kipekee zinazolenga kugusa Maisha ya watu wengi zaidi.”
#KonceptTVUpdates